HOTUBA YA MHESHIMIWA PEREIRA AME SILIMA (MB), MWENYEKITI WA BARAZA LA TAIFA LA USALAMA BARABARANI (T)


HOTUBA YA MHESHIMIWA PEREIRA AME SILIMA (MB), MWENYEKITI WA BARAZA LA TAIFA LA USALAMA BARABARANI (T) KWENYE UFUNGUZI WA MAADHIMISHO YA WIKI YA NENDA KWAUSALAMA BARABARANI KITAIFA MKOANI IRINGA TAREHE 17 SEPTEMBA, 2012

Mhe. Mgeni Rasmi
Mhe. Eng. Gerson  Hosea Lwenge (Mb), Naibu Waziri wa Ujenzi na Makamo Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani
Ndugu Mbarak Abdulwakil, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Ndugu Herbert Mrango, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi
Mhe. Dkt. Christine Ishengoma (Mb), Mkuu wa Mkoa wa Iringa
Ndugu Said Ally Mwema, Inspekta Jenerali wa Polisi
Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Barabarani Mkoa wa Iringa
Wajumbe wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani (T)
Wageni Waalikwa
Wanahabari
Mabibi na Mabwana
Asalaam Aleikum, Amani ya Mungu iwe juu yenu
Awali ya yote napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako Mhe. Mgeni rasmi kwa kukubali kwako  kuungana nasi katika ufunguzi wa wiki ya maadhimisho ya nenda kwa usalama barabarani ambayo kitaifa inaadhimishwa hapa mkoani Iringa.  Kaulimbiu  ya maadhimisho ya mwaka huu ni

“PAMBANA NA AJALI ZA BARABARANI KWA VITENDO, ZINGATIA SHERIA”

Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
Maadhimisho ya Wiki hii yana lengo la kuelimisha na kukumbushana wajibu wa kila mtumiaji wa barabara katika kufuata sheria za usalama barabarani. Ni katika kipindi hiki BARAZA ambacho hufanya maadhimisho haya kwa kuwakusanya wadau mbalimbali wa usalama barabarani kwa ajili ya kujikumbusha au kujifunza. Maonesho huwawezesha wananchi (wadau) kujifunza pamoja na mambo mengine, sheria na kanuni mbalimbali za usalama barabarani. Katika maadhimisho haya wadau watakaoshiriki ni Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Wizara ya Ujenzi, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Scania Tanzania Ltd, Chuo cha Taifa cha Usafirishaji na Mashirika yasiyo ya kiserikali yanayojihusisha na Usalama Barabarani.

Mhe. Mgeni Rasmi,
Tangu nimeteuliwa kuwa Mwenyekiti wa BARAZA hili nimeweza kujionea matatizo na changamoto mbalimbali zinazohusiana na masuala ya usalama barabarani ambazo mimi pamoja na wajumbe wa BARAZA tumekuwa tukikutana mara kadhaa katika kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto zinazotukabili. Suala la usalama barabarani linawahusisha wadau mbalimbali, hivyo kila mdau akitekeleza wajibu wake, ajali za barabarani zitapungua kama sio kumalizika kabisa.

Mhe. Mgeni Rasmi,
Pamoja na jitihada nzuri inayofanywa na Serikali kuboresha Miundombinu ya barabara bado kuna tatizo kubwa la madereva na wapanda pikipiki kutojali Sheria na kanuni za usalama barabarani. Kikubwa kinachochangia ajali hizi ni makosa ya kibinadamu kwa asilimia 78, ubovu wa magari kwa asilimia 12, miundombinu ya barabara kwa asilimia 4 na mengineyo kama moto, hali ya hewa nk kwa asilimia 8.

Katika makosa ya kibinadamu, makosa yanayoongoza ni:-
Mwendokasi
Uzembe wa madereva
Uzembe wa wapanda pikipiki
Uzembe wa wapanda baiskeli
Uzembe wa watembea kwa miguu
Madereva kuendesha magari wakiwa wametumia vilevi

Mhe.  Mgeni Rasmi,
Kwa kuwa makosa ya kibinadamu ndiyo yanayoongoza katika kuchangia ajali nyingi za barabarani, BARAZA la Taifa la Usalama Barabarani likishirikiana na Polisi kikosi cha Usalama Barabarani pamoja na wadau wengine wa usalama barabarani limekuwa na mikakati mbalimbali katika kukabiliana na ajali hizo.

Tumekuwa tukitoa Elimu ya Usalama Barabarani kwa watumiaji wote wa barabara kupitia vyombo vya Habari (Redio na Televisheni).  Hadi sasa kuna jumla ya vituo vya Radio 48 nchi nzima vinavyotumika kutoa elimu ya usalama barabarani.

Kuchapisha vipeperushi vya Elimu ya Usalama Barabarani na kuvigawa maeneo mbalimbali.

Askari wa Usalama Barabarani kwenda katika shule za Msingi na Sekondari kuwafundisha wanafunzi na walimu, kutoa elimu kwa watu mbalimbali wakati wa Maonyesho ya Sabasaba na Nanenane. Aidha, Elimu hutolewa katika Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani.
Kuhakikisha kwamba kila anayeomba Leseni ya Udereva lazima awe amesoma katika Chuo kinachotambulika na Serikali.

Kuhakikisha kwamba madereva wote wa Magari ya Abiria wanakuwa wamesomea na kupata Cheti cha kuendesha magari ya abiria kibiashara (PSV Certificate) toka Vyuo vya NIT na VETA.

Kusisitiza mabasi yote yanayosafiri Masafa marefu kuwa na Madereva wawili wakati wote wa safari.
Askari wa Usalama Barabarani kufanya Doria katika barabara kuu na barabara za ndani ya Mikoa.

kuwashirikisha wananchi katika kutoa taarifa mbalimbali za uvunjaji wa sheria za Usalama Barabarani kupitia Namba za simu za Viongozi wa Polisi zilizopo kwenye Vipeperushi na ile ya Chumba cha Mawasiliano ya Polisi. Aidha, katika mabasi yaendayo mikoani kuna namba za Simu zimebandikwa kwa ajili ya abiria kutoa taarifa ya makosa ya madereva.

Kushirikiana na wadau wa Usalama Barabarani kama Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Uchukuzi, SUMATRA, TANROADS, TBS, BIMA, TABOA, TATOA, DARCOBOA nk. katika kukabiliana na ajali za barabarani na madereva wakorofi wasiotii sheria.

Kuendelea kuishauri Serikali kuifanyia marekebisho Sheria ya Usalama Barabarani ili itoe adhabu kali kwa madereva wasiotaka kufuata sheria. Mhe. Mgeni rasmi kwa sasa sheria ya usalama barabarani inayohusu tozo (notification) imerekebishwa kutoka Tshs. 20,000.00 hadi kufikia Tshs. 30,000.00

Kufuatia kuanza kwa matumizi ya leseni mpya za udereva, utaratibu wa kuweka points katika leseni za madereva wanaofanya makosa utaanza kutumika, ili hatimaye madereva wanaokithiri kwa makosa wanyang’anywe leseni kabisa.

Mchakato wa kuanzisha mfumo wa “Car Tracking” utakaomilikiwa na Serikali upo mbioni kukamilishwa ili kudhibiti mwendokasi wa mabasi yanayosafiri masafa marefu.

Mhe. Mgeni Rasmi,
Ni lengo letu kutekeleza kikamilifu mikakati tuliyojiwekea ili ifikapo 2020 vifo na majeruhi wa ajali za barabarani viwe vimepungua kwa asilimia 50 kama Azimio la Umoja wa Mataifa lilivyoelekeza.

Mhe. Mgeni Rasmi,
Takwimu zinaonyesha kwamba kati ya Januari – Juni, 2012 jumla ya matukio ya ajali 11,163 yaliripotiwa ambapo jumla ya wenzetu 1,808 wamepoteza maisha yao kutokana na ajali hizo. Aidha, jumla ya watu 9,155 walijeruhiwa katika kipindi hicho.Kati ya ajali zote 11,163 zilizoripotiwa, ajali 2,641 ambazo ni sawa na asilimia 24 zimehusisha pikipiki.

Mhe.  Mgeni Rasmi,
Naomba kupitia Hotuba hii kwenye maadhimisho haya ya wiki ya nenda kwa usalama barabarani hapa Mkoani Iringa, niwape pole wafiwa wote waliopoteza wapendwa wao, na wale wote waliopata ulemavu wa maisha kutokana na ajali za barabarani. Aidha, nawaombea pia majeruhi wote kupona haraka ili warudi kwenye kazi zao za kulijenga taifa.

Ndugu Mgeni Rasmi;
Nimalizie hotuba yangu, kwanza kwa kurudia kukushukuru wewe binafsi kwa kukubali mwaliko wetu. Aidha,  niwatake wananchi wote wa Mkoa wa Iringa na vitongoji vyake kuwa na mwamko wa kutembelea maadhimisho haya kwenye viwanja hivi ili waweze kuelimishwa mambo mbalimbali ya usalama barabarani ili  kujikinga na ajali za barabarani.


Mhe. Mgeni Rasmi,
Baada ya kusema hayo, sasa napenda kuchuka fursa hii kukukaribisha ili uweze kutoa nasaha zako .

“PAMBANA NA AJALI ZA BARABARANI KWA VITENDO, ZINGATIA SHERIA”

Mheshimiwa Mgeni Rasmi karibu

Popular posts from this blog

MAMBO 6 YA KUZINGATIA KATIKA MAHUSIANO

Mwanajeshi Aliyepiga Picha na Mbunge wa Arusha Mjini-Chadema Godbless Lema Kwenye Mkutano wa Hadhara Akamatwa

MATAJIRI WATANO WANAOONGOZA TANZANIA