WANAWAKE WANAWEZA KUIPONYA NCHI YETU

MKE wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda amesema wanawake wa Tanzania wanayo nafasi nzuri ya kuungana na kumuomba Mungu ili aiponye nchi hii na majanga mbalimbali. 
 
 
 
 
 
 
“Tutumie nafasi yetu kama wanawake, kuunda jeshi kubwa la maombezi kwa ajili ya nchi yetu. Nchi hii inahitaji maombi, na kwa hakika inamuhitaji Mungu iwe ni kwenye huduma zetu, ndoa zetu, familia zetu na uchumi wetu binafsi na wa Taifa kwa jumla,” alisema.
 
Ametoa kauli hiyo jana jioni (Jumamosi, Juni 9, 2012) wakati akifunga Kongamano la Kitaifa la Wanawake Waombolezao lililodumu kwa siku tatu katika ukumbi wa Sinza Christian Centre jijini Dar es Salaam.
 
Kongamano hilo ambalo liliwajumuisha wanawake 70 kutoka mikoa 31 ya Tanzania Bara na Visiwani na wageni 32 kutoka nchi za Zambia, Zimbabwe, Afrika ya Kusini, Malawi, Uganda, Kenya, na Marekani, lilifunguliwa Juni 7, 2012 na Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Bibi Asha Seif Iddi.
 
“Ninapenda kuwasihi wanawake wote tusichoke kumuomba Mwenyezi Mungu naye atatupa yale tumwombayo. Tusimame kwenye sala na maombi, naye atatusaidia,” alisisitiza.
 
Alitumia fursa hiyo pia kuwaomba akinamama hao wajumuike kuwaombea Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi zaidi ya milioni 45 kwani wanatarajia kuanza kikao cha Bunge Jumanne ijayo.
 
Tumuombe Mungu awaguse Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge ili wabaini kwamba wana jukumu la kuhakikisha wanafanya maamuzi ambayo yatawasaidia Watanzania kujikwamua kutoka kwenye umaskini na hatimaye waweze kupata maisha bora,” alisema.
 
“Sote tunaamini kwamba maombi yaliyofanyika hapa kwa ajili ya viongozi wetu hayataenda bure bali yataleta mabadiliko ndani ya mioyo yao ili wapate ujasiri wa kukataa maovu na kutambua kwamba uongozi walionao ni dhamana waliyopewa na Mungu hivyo wanapaswa kutumia vyema dhamana hiyo kwa ustawi wa Taifa letu.
 
Alitumia fursa hiyo kuwaomba akinamama hao wawaombee Watanzania wote wawe na uzalendo wa kuipenda na kuithamini nchi yao wenyewe, wawe na moyo wa kufanya kazi kwa bidiii na siku zote wawe tayari kuitakia mema nchi hii.
 
Mapema, akitoa mada kuhusu ukomavu wa kiroho, Mwalimu Nikku Kyungu kutoka Marekani alisema wanawake wa Tanzania wanayo nafasi ya kubadilisha mambo kama tu watampa Mungu nafasi ya kutenda na kuacha kuomba kwa mazoea.
 
Mwalimu Kyungu ambaye ni Mtanzania aishiye Marekani ambaye aliokoka tangu akiwa na miaka saba, alisema ana mzigo mkubwa wa kuliombea Bara la Afrika ili watu wake wafunguke na waweze kufaidi rasilmali walizonazo katika nchi zao.
 
Naye Mchungaji Grace Kapswara kutoka Zimbabwe aliwataka akinamama hao wawaheshimu watumishi wa Mungu na wajitoe katika kuwasaidia kama kweli wanataka kufanikiwa maishani mwao.
 
Aliwasisitizia akinamama hao haja ya kuomba kwa pamoja kama timu na kuwaeleza kwamba wakati wao wa kuburudika na kupumzika umekwishawadia.
 
Kongamano hilo la siku tatu liliandaliwa na kanisa la Tanzania Fellowship of Churches chini ya uongozi wa Askofu Godfrey E. Malassy ambaye ni Mwenyekiti wa Mkesha Mkubwa wa Kitaifa.
 

Popular posts from this blog

MAMBO 6 YA KUZINGATIA KATIKA MAHUSIANO

CATHERINE MASUMBIGANA AWA REDD'S MISS CHANG'OMBE

HOTUBA YA MHESHIMIWA PEREIRA AME SILIMA (MB), MWENYEKITI WA BARAZA LA TAIFA LA USALAMA BARABARANI (T)